Friday, June 3, 2011

HARUSI ZA KIAFRIKA: NANI KASEMA HATUNA UBUNIFU?

Nani kasema hatuna ubunifu? Nani kasema watanzania hawana kitu cha kujivunia.

kwa kipindi kifupi nilichokaa Tanzania baada ya kuishi Uingereza takribani miaka tisa nimegundua kuwa watanzania ili suala la kuchangishana na kusherehekea harusi ni la kwetu, halipo Ulaya. Made in Tanzania.

Lina faida? Nyingi tu, na ninawabeza wanaochoka na kudai kuwa ni uchomaji wa pesa, eti tunachangishana mno na kuchoma pesa kwa siku moja. Kwanini tusifanye hivyo? Je, nyie mnaotushangaa hamjui siye ni matajiri.

Watanzania tunaoishi mijini, hasa Dar Es Salaam tuna mtazamo wa mashambani ambalo nalo si jambo baya, ni zuri tu, na hapo ndipo inapopendeza tunaleta mapokeo ya kijijini mjini na kufanya sherehe za harusi ziwe za kula, kunywa, na kusaza. Si ndiyo ilivyo kijijini? Ndiyo bwana ndivyo tulivyolelewa. Kwa miye mwenyeji wa Kagera, kule kwetu enzi zile ndizi hazijaingiliwa na wadudu, tulikuwa tunatengeneza pombe nyingi sana, kunywa, kula matoke mpaka kuvimbiwa. Watanzania/waafrika kwa ujumla ni watu wa kusaza bwana.

Sasa tunapokuja mijini, pesa ni ngumu, ni ngumu kwa mtu mmoja kuitisha pombe na kufurahisha mamia ya watu, na hapo ndipo unapokuja umuhimu wa kuchangishana katika kusherehesha harusi ya Bwana na Bibi harusi.

Na hata mipangilio mizima ya harusi inaonyesha ubunifu mkubwa. Kuna Mwenyekiti, katibu, mweka hazina( huyu anaaminika tu kwa uaminifu wake) na inapokaribia siku ya harusi, kamati zinaundwa; kama vile kamati ya vinjwaji, kamati ya ulinzi, kamati ya chakula, floor manager, nk.

wajumbe wa kamati huwa wanafanya kazi kwa uadilifu mkubwa na bidii kubwa hili kufanikisha siku yenyewe na kwa kweli wanastahili sifa maana hakuna mishahara, na kujitoa kwa ukweli na hakika siku ya mwisho Bwana na Bi Harusi wanakuwa wamesaidiwa na marafiki na ndugu wa ukweli.

Suala la kufahamiana je, waingereza wanaita 'contacts'. Hapa mjini kama nyie mlio ulaya hamjui kufahamiana ndio mwendo murua. Hapa bila kujua mtu, maisha hayasongi mbele. Sasa kwenye vikao vya harusi, na tu 'deal' tudogo tudogo na hata madeal makubwa ndipo yanapofanyika. Kwa kipindi kifupi nilichohudhuria vikao vya harusi nimeweza kupata marafiki wengi wanaonipa fursa mbalimbali za kuyamudu maisha ya Dar. Business cards zitatolewa, namba za simu mtapeana, na hata mchumba unaweza kumpata kwenye hivi vikao kwa wale ambao bado hawajaoa. Vikao vya harusi navyo ni 'business forum' hisiyo rasmi, lakini ya kibongo bongo.

Muhimu zaidi ni hili suala la kupigana tough, waingereza wanasema 'scratch my back, I will scratch yours. Unapomchangia mtu harusi leo hatakusahau, huwezi kujua kesho utakwenda pale hospitali ya muhimbili na matatizo ya ngiri na utamkuta dactari ndio yule yule uliemchangia harusi yake, bingo, umepata matibabu.

Ingawa naupigia upatu utaratibu huu, ningependelea tuweke vionjo ya kimagharibi ili kupendezesha na kufanikisha huu ubunifu wetu. Swali linanijia kichwani, mbona serikali yetu haioni hiki kama kiwanda na kukitoza kodi?? Michango ya harusi inatengeneza pesa, kwanini isitozwe kodi na manufaa ya maendeleo ya watanzania wote?

Najua wameanza kutoza ushuru wenye kumbi za harusi, ndio ni vyema kabisa. Je hisingekuwa vyema tukaenda mbali zaidi na kutoza ushuru vikao vya harusi?? labda michango ya harusi ndio 'Toyota' yetu? Nani kasema watanzania hatuna bidhaa.

Tufike mahali labda tuseme harusi inayozidi bajeti ya million kumi itozwe kodi asilimia fulani!!! je, haiwezekani unapoenda kutoa 'order' ya keki, ukalipishwa VAT?(value added tax). Pesa zinazopatikana kutokana na michango ya harusi inaweza kusaidia utengenezaji wa barabara, ujenzi wa zahanati na hata kujenga mashule. Ni pesa inayozunguka humu ndani kwa ndani ambayo mamlaka ya Kodi haijaing'amua bado.

Msinichukie jamani, nami natamani nasi tuwe na bidaa za kujivunia zinazoweza kutozeka kodi.

2 comments:

  1. hilo wazo Ni zuri na mm naliunga Mkono...Ila Je ushwahi Jiuliza Watanzania na serikali yake wana Njia nyingi ya kujipatia hela kwa kutoza kodi Ila bado hali yetu ni duni...Pesa zinazopatiKana kutoka kwenye hizo kodi hutmika kujAza matumbo ya wa2 wachache huku hali ya watu wengi kuwa taaban kama mgonjwa wa T.B...jaMbo la msingi ni kuomba na kupata viongozi wenye Utashi na wasio na mawazo finyu Ili waweze kusimamia njia hizo na kutumia kodi hizo kuboresha maisha ya Mtanzania au mwafrika yoyote kwani akili za baadhi ya viongozi we2 hapa afrika zinafanana kama rangi ye2...

    ReplyDelete
  2. Na Pia suala la kuiga manjonjo ya Kimagharibi kwa upande wangu naona kama tutakuwa tunatoka na kuacha tamaduni zetu za kiafriika na kukimbilia huko kwa watu weupe(magharibi) jambo ambalo nalipinga vikali ni sawasawa kuweka rangi kwenye maziwa ambayo matokeo yake mwishowe maziwa yanakuwa na rangi unayosema ww manjonjo ya kimagharibi....ubunifu wa Jambo sio lazima Utumie tamaduni za wengne ila waweza tumia tamaduni yako hyo hyo kuboresha hali flani iwe bora zaidi

    ReplyDelete